Header AD

JOHN KOMBA AONGELEA KUHUSU AFYA YAKE......


Mkurugenzi wa  Tanzania One Thetre (TOT) ambaye pia ni Mbunge wa Mbinga Magharibi, John Komba akizunguma na waandishi wa habari nyumbani kwake, Mbezi Tangi Bovu, Kawe, Dar es Salaam, leo  wakati akizungumzia hali ya afya yake baada ya kurejea nchini akitoka nchini India alikokwenda kufanyiwa upasuaji. Kushoto ni Mkewe, Salome Andrew Komba. 
**********************************
NA BASHIR NKOROMO

MKURUGENZI wa Kundi la Tanzania One Theatre (TOT) ambaye pia ni Mbunge wa Mbinga Magharibi, John Komba amerejea kutoka India ambako amefanyiwa upasuaji kumtibu ugonjwa wa nyonga ulilokuwa ukimsumbua upande wa mguu wake wa kulia.

Akizungumza na waandishi wa habari, jana Julai 27, 2012, nyumbani kwake Mbezi kwa Komba, mjini Dar es Salaam, Komba alisema amerejea nchini,  Juzi,  baada ya kupatiwa matibabu hayo kwenye hospitali ya Appolo iliyopo Hydrabad nchini India tangu mwanzoni mwa wezi huu.

Alisema, aliondoka nchini, Julai 2, 2012, baada ya kupelekwa na serikali kwa maelekezo ya Rais Jakaya Kikwete, Spika wa Bunge Anna Makinda na Katibu wa Bunge John Kashilila na kwamba alikwenda baada ya kukosa matibabu hapa nchini kwa sababu ya mgomo wa madaktari.

"Siku napelekwa Muhimbili tu, tayari madaktari walikuwa wameanza siku ya kwanza ya mgomo wao, nikawa sina namna ila kuujulisha uongozi wa Bunge na kisha nikamuomba Mwenyekiti wa CCM, Rais Jakaya Kikwete, naye kwa mamlaka yake akanisaidia haraka kama ambavyo huwasaidia wengine kwenda kutibiwa nje", alisema Komba.

Alisema, uzito ulichangia sana kusababisha mifupa kusagana kwenye nyonga upande wa mguu wa kulia, ambapo hadi anakwenda India alikuwa na uzindo wa kilo 138 wakati wastani wa uzito aliotakuwa kuwa nao kulingana na ukumbwa wa mwili wake ni kilo 90 au 100 tu.

"Amesema, baada ya matibabu amerejea nchini akiwa na uzito wa kilo 128 ambao hata hivyo ametakiwa kuudhibiti na kuupunguza katika siku hizi ambazo atalazimika kupumzika nyumbani kabla ya kuanza kazi, Mwezi Septemba mwaka huu kama alivyoelekezwa na madaktari.

Akizungumzia upasuaji ulivyoendeshwa, Komba alisema, ulichukua saa tano na kukamilika bila matatizo katika upasuaji huo ambao alisema sehemu iliyopasuliwa ni ya ukumbwa wa futi moja.

Alisema, hata hivyo baada ya upasuaji huo, hakuweza kurejea katika wodi ya kawaida, kwa sababu majongwa kadhaa yaliibuka ikiwemo homa kali, presha, hivyo akalazimika kulazwa katika wodi ya wagonjwa waliopo kwenye uangalizi maalum (ICU) kwa siku tano.

"Sasa nimerejea nikiwa mzima, kwa sasa natumia fimbo hii, ili kuwezesha uzito uzilemee upande wa kulia nilikopanyiwa upasuaji, lakini sijambo kabisa", alisema Komba.

Komba alilaani baadhi ya vyombo vya habari ambavyo viliripoti kwamba katika kuugua kwake alikuwa mahututi na kwamba alikuwa anaugua figo.

"Jamani ninyi waandishi wa habari, jizoesheni kuandika habari zilizokamilika siyo kurashia-rashia tu na kuzusha uongo, mfano gazeti moja liliandika eti naugua figo nipo mahututi, wakati si kweli kabisa, ilikuwa jambo rahisi tu, kuja hapa nyumbani na kuniuliza au kuuliza mke wangu lingepata kwa uhakika ninachoumwa", alisema Komba.
Reviewed by crispaseve on 12:04 Rating: 5

No comments

Post AD