TPC YAFIKIA VIWANGO VYA UBORA WA HUDUMA KIMATAIFA
Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi ya SHIRIKA la Posta Tanzania, Dr.
Yamungu Kayandabila (katikati) na Postamasta Mkuu Bw. Deos Mndeme
(kushoto) wakipokea cheti maalum kuashiria kufikia viwango vya utoaji
wa huduma bora za kimataifa za Posta. Anayekabidhi cheti ni Mkurugenzi
Mkuu wa Umoja wa Posta Duniani Bw. Eduard Dayan
Na Innocent Mungy, Doha Qatar
Viwango vya huduma zinazotolewa na SHIRIKA la Posta Tanzania (TPC), vimekidhi viwango vya Shirika la Umoja wa Posta Duniani (Universal Postal Union-“UPU”).
UPU leo imetoa cheti maalum kwa Shirika la Posta Tanzania kuwa miongoni mwa Mashirika wanachama waliofikia viwango vya juu vya utoaji wa huduma za Posta kwa Tanzania na nchi zote zinazoshirikiana na TPC kwa huduma za Posta kote ulimwenguni. Shirika la Posta limepata alama 1,765 kati ya alama 2000 zinazotakiwa, ambazo ni za juu kulinganisha na nchi zingine.
Kamati
ya UPU inayosimamia Masuala ya Upimaji wa Ubora wa Huduma (Quality of
Service Improvement Group Steering Committee) iliridhika na kasi,usalama na ufuatiliaji wa huduma za kusafirisha barua,nyaraka na vipeto zinazotolewa na Shirika la Posta Tanzania.
Cheti hicho cha kuthibitisha Ubora wa Huduma zinazotolewa na TPC, kilikabidhiwa kwa Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi wa
Shirika la Posta Tanzania Dr. Yamungu Kayandabila leo jijini Doha,
Qatar mbele ya Mkutano Mkuu wa Kamati Namba 7 ya UPU inayoshughulikia
Huduma na Masoko.
Akizungumza jijini hapa baada ya kupokea cheti
hicho, Dr. Kayandabila amesema cheti hicho ni ushahidi wa dhamira ya
Bodi ya Wakurugenzi, Menejimenti na Wafanyakazi wa Posta kuhakikisha
wanatoa huduma bora na zenye kukidhi viwango vya kimataifa kama nchi
zilizoendelea duniani.
Naye Postamasta Mkuu wa SHIRIKA la Posta
Tanzania, Bw. Deos Mndeme ameelezea furaha yake kwa Shirika kufikia
viwango vilivyowekwa na UPU, aidha amewashukuru na kuwapongeza Wafanyakazi wote wa Shirika la Posta Tanzania kwa kazi nzuri wanayoendelea kufanya na kuliwezesha Shirika
kutimiza viwango vya utoaji wa huduma za Posta hususan usambazaji wa
barua,nyaraka,vifurushi na vipeto hadi kufikia viwango vinavyokubalika
kimataifa.
"Shirika
la Posta linawahakikishia Watanzania na watumiaji wa huduma zetu kote
duniani kuwa tutaendelea kutumia mazingira mapya na teknolojia za kisasa katika kuboresha huduma huku tukizingatia mkakati mpya wa utoaji wa huduma za Posta Duniani", Alisema Bw. Mndeme.
Aidha
Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania Prof. John Nkoma
amesema Tanzania kufikia viwango hivyo vya UPU ni jambo zuri na la sifa
kubwa kwa nchi, lakini pia changamoto kwa Shirika la Posta ambalo
halina budi kuhakikisha kuwa linaendelea kukidhi viwango hivyo siku zote
kwa manufaa ya watumiaji wa huduma za Posta nchini na kwingineko
kutokana na huduma hizi hutolewa kati ya Tanzania na nchi zingine.
"Sisi
TCRA kama wasimamizi wa sekta ya Mawasiliano, zikiwamo huduma za
Posta, tutaendelea kusimamia kuhakikisha viwango walivyofikia
wanavidumisha ili kukidhi matakwa ya huduma bora kwa wateja kwa mujibu
wa kanuni na sheria lakini pia na matarajio ya watumiaji huduma za
Posta", alisema Prof. Nkoma.
Shirika la Posta Tanzania limepitia
mchakato maalum wa Umoja wa Posta Duniani ili kuthibitisha kuwa
limefikia viwango vinavyokubaliwa na nchi wanachama wa Umoja huo, na
sasa ni miongoni mwa Mashirika yanayoaminika duniani kwa utoaji wa
huduma za Posta zinazokidhi viwango vya kimataifa.

Post a Comment