Header AD

mtu mmoja anaendelea kuhojiwa na polisi kufuatia mlipuko wa bomu arusha


Waumini wakiwa katika taharuki kufuatia mlipuko huo wa bomu jijini Arusha leo. Chini makachero wa polisi wakifanya uchunguzi eneo la tukio.
Baba Askofu Mkuu wa Jimbo la Kanisa Katoliki Arusha, Mhashamu Josephat Louis Lebulu na Mwakilishi wa Papa, Nuncio, Francisco Montecillo Padilla kabla ya mlipuko huo. Viongozi hawa wa dini walinusurika na waliondolewa haraka eneo la tukio na wasaidizi wao wakiwa salama
Taharuki mara baada ya mlipuko huo wa bomu.Picha na Woinde Shizza

Na Ahmed Mahmoud

MTU mmoja amekamatwa na anaendelea kuhojiwa na polisi kufuatia mlipuko mkubwa wa bomu lililorushwa kwa waumini wa Kanisa Katoliki jana ambapo watu 66 wamejeruhiwa wakiwamo wanawake 41 na wanaume 25, huku majeruhi wawili hali zao zikiwa mbaya zaidi.

Mkuu wa Mkoa wa Arusha, Mhe Magesa Mulongo alimweleza Makamu wa Rais, Dk. Mohamed Gharib Bilal na Mkuu wa Jeshi la Polisi nchini, IGP Saidi Mwema,Naibu waziri wa mambo ya ndani Mhe Pereira Silima,na Naibu Waziri wa Nishati na Madini  Mhe Stephen Masele wakati walipowatembelea majeruhi waliolazwa katika Hospitali ya Mount Meru jana jioni.
Alisema kati ya majeruhi hao, wawili hali zao ni mbaya, huku mmoja akiwa akiwa amepelekwa hospitali ya KCMC kwa matibabu zaidi.
Makamu wa Rais alitarajiwa kuondoka na majeruhi mwingine mtoto ambaye anapelekwa Hospitali ya Taifa ya Muhimbili kwa matibabu zaidi.

RC Mulongo alithibitisha kwamba aliyefariki katika tukio hilo ni mama mmoja wa kwanya ya Kimasai ambayo ilikuwa ikiimba kwenye shughuli za uzinduzi wa kanisa hilo.

Akitoa pole kwa wagonjwa waliolazwa pia kwa wale ambao jamaa zao wamepata maradhara kwa tukio hilo, kwa waumini wa Kanisa Katoliki, kwa wakazi wa Arusha na Watanzania kwa ujumla, Dk Bilal alisema tukio hilo ni la aibu na baya sana. “Tukio hili ni la aibu sana, baya, limeshtusha kutokea hapa nchini, serikali inalaani na itafanya kila linalowezekana kuwatia mbaroni wahusika na tayari imekwishaanza kuhakikisha wahusika wanakamatwa.

“Vyombo vya usalama vimeagizwa kufanya kazi hii usiku na mchana kuhakikisha kwamba wahusika wanakamatwa na wanachukuliwa hatua,” alisema.
Mkuu wa Jeshi la Polisi, Mwema akitokea Dodoma kuhudhuria vikao vya bunge ambako leo Wizara ya Mambo ya Ndani inawasilisha bajeti yake, alielezea tukio hilo kuwa ni la kushutua sana.
“Ni tukio la kushtua, kusikitisha, tumefika eneo la tukio na mpaka sasa mtu mmoja amekamatwa na anaonyesha ushirikiano mzuri wa kutoa taarifa.

“Tukio kama hili sio la mtu mmoja, wapo waliohusika katika kupanga, kuratibu, kushauri, kuchangia gharama na wale waliofanikisha. Hata huyu mmoja aliyekamatwa ni mchango wa ushirikiano wenu, naombeni muendelee kushirikiana na polisi katika kufanikisha uchunguzi huu.
Kwa upande wake, Askofu Mkuu wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri  Tanzania (KKKT), Dk Alex Malasusa, ambaye aliambatana na Makamu wa Rais kutokea mkoani Shinyanga, alisema amesikitishwa sana na tukio hilo.
Alisema tukio hilo sio la kawaida na limewashtua watu wengi wanaopenda amani lakini amewaomba waendelee kuwa watulivu wakati suala hili linapoendelea kufanyiwa uchunguzi. “Wakristo tuendelee kuhubiri amani, kuombea amani kwa sababu Mungu wetu ni wa amani,” alisema.


Majina ya waliojeruhiwa katika tukio hilo ambao wamelazwa katika hospitali za  mount Meru, na hospitali teule ya jiji la Arusha ya St Elizabeth wametambulika kuwa ni:-  

John Thadei, Regina Fredirick, Joram Kisera, Novelt John, Rose  Pius, John  James, Anna Kessy, Joan Temba, Neema Kihisu, Gloria Tesha, Innocent Charles, Fatuma Haji, Fikiri Keya, Simon Andrew, Anna Edward, Lioba Oswald, Rose Pius, Philemon Gereza,Kisesa Mbaga na Beata Cornell.  Majeruhi wengine na umri wao katika mabano, ni Consensia Mbaga (53), Christopher Raymond (10), Deborah Joachim (24), Elizabeth Isidori (24), Anna Didas (52), Bertha Cosinery (49), Edda Ndowo (77), Derick Cyprian (8), Faustine Andrea (35), Mary Okech, Mesoit Siriri (33), Clenes pius (22), Joyce yohana (15), Restituta Alex (50), Mathias Riha (74), Magreth Andrew(45), James Gabriel (16), Regina James (17),Elizabeth Masawe(15), Elizabeth Sauli (18), Njau (35), Yasinta Msafiri (16) Doreen Pancras (28), Alex Arnold, Agripina Alex (9), James Gabriel (16), Loveness Nelson (17), Amalone Pius (25), Frank Donatus (10), Alphonce Nyalandu (26), Athanasia Reginald (14), Phillemon Ceressa (49), Neema Daud (13), Sophia Kanda (72), Theofrida Innocent (21) na Regina Darnes(17).

Rais kikwete alaani shambulio la kigaidi arusha, aagiza waliohusika wasakwe na kufikishwa mbele ya sheria


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete amepokea kwa mshtuko na masikitiko makubwa taarifa ya tukio la leo, Jumapili, Mei 5, 2013 la mlipuko kwenye Kanisa Katoliki la Mt. Joseph Mfanyakazi la Olasiti Jijini Arusha.  Tukio hilo la kigaidi limesababisha mtu mmoja kupoteza maisha na wengine 40 kujeruhiwa.  

Rais Kikwete analaani vikali shambulio hilo lililofanywa na mtu au watu
katili, waovu na wenye dhamira mbaya na nia mbaya kwa Tanzania na watu
wake. 

Rais Kikwete ameagiza vyombo vya usalama nchini kumsaka mtu au watu waliohusika na kitendo hicho kiovu na kuwafikisha kwenye vyombo vya sheria.  Vile vile Rais Kikwete amewataka wananchi wote kuwa watulivu wakati Serikali na vyombo vyake inaendelea kufuatilia tukio hili.  

"Tutawasaka popote walipo na kupambana nao bila huruma.  Aidha, tutakabiliana na aina yoyote ya uhalifu nchini iwe ni ugaidi au aina yoyote ya uhalifu wa namna hiyo au wa namna nyingine, uwe na chimbuko lake ndani ya nchi ama nje ya nchi yetu.   "Kamwe hatutakubali kuwaacha wavuruge amani na usalama wa Tanzania na watu wake" amesema Rais ambaye anaamini kuwa Serikali, kwa msaada na ushirikiano wa wananchi, watu hao watapatikana na kuadabishwa ipasavyo. Aidha, Rais Kikwete anatoa rambirambi za dhati ya moyo wake kwa wafiwa na wale wote ambao wamejeruhiwa katika tukio hilo. Anaungana nao katika machungu na msiba. Rais pia anawaombea wote walioumia katika tukio hili wapate nafuu ya haraka na waendelee na shughuli zao za ujenzi wa taifa.

Rais Kikwete vilevile anatoa pole nyingi kwa viongozi na waumini wa Kanisa Katoliki kwa tukio hili la kusikitisha na kuvurugika kwa ibada na shughuli yao muhimu ya uzinduzi wa Kanisa lao.


Imetolewa na:
Kurugenzi
ya Mawasiliano ya Rais,
IKULU,
DAR ES SALAAM
Reviewed by crispaseve on 05:23 Rating: 5

No comments

Post AD