Hotuba ya Rais wa Jamuhuri ya Muungano wav Tanzania Wakati akilihutubia Bunge Maalum la Katiba Mjini Dodoma leo jioni.
HOTUBA YA RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA, MHESHIMIWA JAKAYA MRISHO KIKWETE,
WAKATI WA KULIHUTUBIA BUNGE
MAALUM LA KATIBA, TAREHE 21 MACHI, 2014, DODOMA
RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA, MHESHIMIWA JAKAYA MRISHO KIKWETE,
Mheshimiwa
Samuel Sitta, Mwenyekiti wa Bunge Maalum la Katiba;
Mheshimiwa
Dkt. Mohamed Gharib Bilal, Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania;
Mheshimiwa
Dkt. Ali Mohamed Shein, Rais wa Zanzibar
na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi;
Mheshimiwa
Mizengo Peter Pinda, Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania;
Mheshimiwa
Maalim Seif Sharif Hamad, Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar;
Mheshimiwa
Balozi Seif Ali Iddi, Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar
Mheshimiwa
Anne Semamba Makinda; Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano;
Mheshimiwa
Pandu Ameir Kificho, Spika wa Baraza la Wawakilishi na Mwenyekiti wa Muda wa
Bunge Maalum la Katiba ;
Mheshimiwa
Rashid Othman Chande, Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania;
Mheshimiwa
Othman Makungu, Jaji Mkuu wa Zanzibar;
Viongozi
Wakuu Wastaafu;
Waheshimiwa
Wajumbe wa Bunge Maalum la Katiba;
Waheshimiwa
Wajumbe wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba;
Wageni
waalikwa;
Mabibi
na Mabwana;
Pongezi
Nakushukuru
sana Mheshimiwa
Mwenyekiti kwa kunipa fursa ya kuja kuzungumza na Waheshimiwa Wajumbe wa Bunge
letu Maalum la Katiba katika siku hii muhimu na ya kihistoria kwa nchi yetu. Nimekuja kuwatakia heri na naungana na
Watanzania wenzetu wote kuwaombea baraka za Mwenyezi Mungu, ili muweze kuifanya
kazi yenu kwa utulivu, hekima, umakini mkubwa na kuimaliza kwa salama na kwa
mafanikio yanayoyatarajiwa na Watanzania.
Natoa pongezi nyingi kwako na
kwa Makamu wako kwa kuchaguliwa kwenu kuongoza Bunge hili maalumu na la
kihistoria. Ushindi mkubwa mliopata ni
kielelezo tosha cha imani kubwa na matumaini waliyonayo Wajumbe wenzenu kwenu. Matumaini
yao ndiyo matumaini ya Watanzania wote, kwamba
mtaliongoza vizuri Bunge hili, ili liweze kutimiza kwa ufanisi mkubwa jukumu lake muhimu sana katika historia ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Mheshimiwa Mwenyekiti;
Niruhusu pia niwapongeze kwa dhati
Wajumbe wote wa Bunge Maalum la Katiba kwa bahati ya aina yake waliyopata ya
kutunga Katiba mpya ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Fursa hii hutokea mara chache sana katika historia ya nchi yo yote na watu
wake. Mkifanikiwa kuipatia nchi yetu
Katiba nzuri majina yenu yataandikwa kwa wino wa dhahabu, katika kumbukumbu za
historia ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Ni matarajio ya Watanzania
kuwa mtatunga Katiba itakayokubalika na wengi.
Katiba inayotekelezeka. Katiba
itakayoimarisha Muungano wetu kwa kuondoa changamoto zilizopo sasa. Katiba itakayoipa nchi yetu mfumo bora wa kuongoza
na kuendesha mambo yetu. Katiba
itakayoimarisha umoja, upendo, ushirikiano na mshikamano miongoni mwa wananchi
wa Tanzania,
licha ya tofauti zao za asili za upande wa Muungano na maeneo watokako, au tofauti
za jinsia, rangi, kabila, dini na ufuasi wa vyama vya siasa. Katiba itakayodumisha amani, usalama na
utulivu nchini. Katiba itakayostawisha zaidi
demokrasia, haki za binadamu, utawala wa sheria, utawala bora na kudhibiti
maovu.
Na, mwisho ingawaje siyo
mwisho kwa umuhimu, Katiba itakayoweka mazingira mazuri kwa uchumi wa nchi
kukua, na wananchi wengi kunufaika sawia na maendeleo yatayopatikana.
Historia
ya Katiba Nchini
Mheshimiwa Mwenyekiti na Waheshimiwa
Wajumbe;
Hii itakuwa mara ya tatu
tangu kuzaliwa kwa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Aprili 26, 1964, kwa nchi
yetu kuwa na mchakato wa kutunga Katiba mpya.
Mara ya kwanza ilikuwa mwaka 1965 ilipotungwa Katiba ya Muda na mara ya
pili ni mwaka 1977 ilipotungwa Katiba ya Kudumu tuliyonao sasa. Tofauti na mara mbili zilizopita, safari hii
mchakato unahusisha watu wengi zaidi. Wananchi
wameshiriki moja kwa moja kutoa maoni yao
kwa Tume ya Mabadiliko ya Katiba, na ndio watakaofanya uamuzi wa mwisho kuhusu
Katiba mpya kwa kura ya maoni. Wananchi
pia walipata nafasi ya kuchagua Wajumbe wa Mabaraza ya Katiba ya Wilaya yaliyojadili
Rasimu ya Kwanza ya Katiba. Pia walipata nafasi ya kutoa maoni yao kupitia Mabaraza ya Katiba
ya taasisi. Katika Bunge hili wapo
wananchi 201 kutoka makundi
mbalimbali.
Katika mchakato wa kutunga
Katiba za mwaka 1965 na 1977 kulikuwapo Tume za Kuandaa Rasimu na Bunge Maalum
la Katiba kama ilivyo katika mchakato
huu. Hata hivyo, kwa Katiba zilizopita
Wabunge wa Bunge la Jamhuri ya Muungano pekee ndio waliounda Bunge Maalum. Safari hii Bunge Maalum linajumuisha Wabunge,
Wajumbe wa Baraza la Wawakilishi na wananchi 201 wanaotoka kwenye jamii,
wakiwakilisha asasi na makundi mbalimbali ya Watanzania kutoka Zanzibar na Tanzania Bara. Mchakato wa sasa utaishia kwenye kura ya
maoni itakayoshirikisha wananchi wote wa Tanzania wanaoruhusiwa kupiga
kura. Michakato iliyopita iliishia Bunge
Maalum pekee.
Mheshimiwa Mwenyekiti;
Tangu kutungwa kwake, tarehe
25 Aprili, 1977, mpaka sasa Katiba ya Jamhuri ya Muungano ya mwaka 1977
imefanyiwa mabadiliko takriban mara 14.
Mabadiliko hayo yalitokana na kufanyika au kutokea kwa mabadiliko muhimu
ya kiuchumi, kisiasa na kijamii katika nyakati mbalimbali hapa nchini na katika
Jumuiya ya Afrika Mashariki.
Kwa ruksa yako naomba nitaje
baadhi ya mabadiliko yaliyofanywa:-
1. Mabadiliko
ya 1979 yaliunda Mahakama ya Rufani ya Tanzania kufuatia kufa kwa Mahakama
ya Rufani ya Afrika Mashariki baada ya kuvunjika kwa Jumuiya ya Afrika
Mashariki mwaka 1977.
2. Mabadiliko
ya mwaka 1980 yalifanyika baada ya kutungwa kwa Katiba ya Zanzibar, hivyo kulazimu Katiba hiyo
kutambulika kwenye Katiba ya Jamhuri ya Muungano.
3. Mabadiliko
ya mwaka 1984 yaliweka utaratibu wa ukomo wa vipindi vya Urais ambao haukuwepo
kabla ya hapo. Aidha, masuala ya Haki za
Binadamu (Bill of Rights) yaliingizwa kwa mara ya kwanza katika Katiba. Vilevile,
Mahakama ya Rufani ya Tanzania
na mambo mengine ya iliyokuwa Jumuiya ya Afrika Mashariki yaliongezwa katika
Orodha ya Mambo ya Muungano.
4. Mwaka
1992, yalifanyika mabadiliko yaliyoanzisha Mfumo wa Vyama Vingi vya Siasa
badala ya ule wa Chama kimoja uliokuwepo tangu 1965. Pia utaratibu wa uchaguzi wa Rais na Wabunge
ulirekebishwa ili uendane na mfumo wa vyama vingi vya siasa. Vilevile utaratibu wa kuwa na viti maalum vya
wanawake katika Bunge ulianzishwa. Wakati ule ilikuwa asilimia 15 ya Wabunge
wote. Aidha, kwa mara ya kwanza katika
historia ya nchi yetu Bunge lilipewa mamlaka ya kumwajibisha Rais na Waziri
Mkuu kupitia kura ya kutokuwa na imani.
5. Mabadiliko
ya mwaka 1994 yaliweka mfumo mpya wa kumpata Makamu wa Rais kupitia Mgombea
Mwenza.
6. Mwaka
2000 na 2005, pamoja na mambo mengine yalifanyika mabadiliko yaliyopanua wigo
wa Haki za Binadamu na kuongeza
uwakilishi wa wanawake.
Umuhimu
wa Mabadiliko ya Katiba
Mheshimiwa Mwenyekiti;
Kufanyika kwa mabadiliko hayo
kunathibitisha utayari wa Serikali kufanya mabadiliko kila ilipoonekana inafaa
kufanya hivyo. Pamoja na kufanya yote hayo
na Serikali kuwa na msimamo huo, kumekuwepo na madai yaliyokuwa yanajirudia ya
kutaka Katiba ya Tanzania
iandikwe upya. Wako watu walioimithilisha
Katiba yetu na nguo yenye viraka vingi mno kiasi kwamba ingefaa kununua mpya
badala ya kuendelea kuivaa.
Madai ya kutaka Katiba mpya yalipazwa sauti
baada ya kuanza kwa mfumo wa vyama vingi vya siasa. Wapo waliokuwa wanadai Katiba mpya kwa imani,
eti kwamba, itawawezesha kuishinda CCM.
Lakini, si hayo tu, hata katika mchakato wa Serikali zetu mbili kushughulikia
kero za Muungano, imedhihirika kuwa baadhi ya changamoto zilikuwa zinahitaji mabadiliko
ya Katiba ili kuzipatia ufumbuzi wa uhakika na wa kudumu.
Mheshimiwa Mwenyekiti;
Kwa kutambua ukweli huo na baada
ya kushauriana na kukubaliana na viongozi wenzangu wakuu wa Chama tawala na
Serikali zetu mbili wakati ule, ndipo tarehe 31 Desemba, 2010, nikatangaza dhamira
ya kuanzisha mchakato wa kutunga Katiba mpya.
Nilieleza siku ile kuwa katika mchakato huo tutakuwa na ushirikishwaji
mpana wa wananchi wa Tanzania
kwa makundi yao
ya jinsia, dini, siasa na shughuli wazifanyazo kujipatia riziki na kwa maeneo
wanayotoka katika pande zetu mbili za Muungano.
Hotuba ya Rais wa Jamuhuri ya Muungano wav Tanzania Wakati akilihutubia Bunge Maalum la Katiba Mjini Dodoma leo jioni.
Reviewed by crispaseve
on
05:49
Rating:
Post a Comment