Header AD

Tume ya Katiba yafafanua ukomo wa wananchi kutoa maoni

Na Mwandishi Wetu
Tume ya Mabadiliko ya Katiba imetoa ufafanuzi kuhusu malalamiko ya baadhi ya wananchi kuwa Tume hiyo imeweka ukomo wa idadi ya wananchi wanaotoa maoni katika mikutano yake inayoendelea katika mikoa minane na kuwaomba wananchi kuendelea kujitokeza kwa wingi katika mikutano inayoitishwa na Tume na kutoa maoni yao kwa uhuru na uwazi.

Katibu wa Tume hiyo Bw. Assaa Rashid amesema leo (Jumapili, Julai 8, 2012) kuwa Tume ingependa kupata maoni ya kila mwananchi na hivyo haiwezi kuweka ukomo kwa wananchi kutoa maoni katika mikutano inayoiitisha.

Ufafanuzi wa Tume hiyo unafuatia taarifa kupitia vyombo mbalimbali vya habari zikinukuu baadhi ya wananchi wakilalamika kuwa Tume ya Mabadiliko ya Katiba imeweka kikomo cha idadi ya maswali na watu wanaotakiwa kutoa maoni yao katika mikutano ya kukusanya maoni ya wananchi.

Taarifa hizo ziliongeza kuwa Tume ya Mabadiliko ya Katiba imekuwa ikitoa nafasi kumi tu kwa wananchi wanaopaswa kuuliza maswali yasiyozidi kumi katika mkutano mmoja na kwamba, katika baadhi ya Wilaya, ikiwemo Biharamulo yenye Kata 15, ni Kata sita tu ndizo zilizofikiwa na Tume.

“Katika baadhi ya Wilaya, kama Kusini Unguja na Bahi mkoni Dodoma, Tume imelazimika kuongeza muda wa kupokea maoni ya wananchi na wakati mwingine kuongeza idadi ya mikutano hadi kufikia mitatu badala ya miwili kwa siku. Hatua hizi zinalenga kutoa fursa zaidi kwa wananchi kutoa maoni yao,” amesema Bw. Assaa katika taarifa yake kwa vyombo habari. 

Kuhusu mikutano iliyofanyika wilayani Biharamulo, Bw. Assaa amesema Tume ilipanga na imefanya mikutano sita kuanzia terehe 2 hadi 4 Julai, 2012 na jumla ya wananchi 267 walitoa maoni yao kwa mdomo na wananchi wengine 265 walitoa maoni yao kwa maandishi.

Kwa mujibu wa katibu huyo, vituo ambavyo mikutano hiyo ilifanyika ni Kelenge, Movata, Nyamigogo, Runazi, Nyakanazi na Biharamulo Mjini.

“Katika mikutano hiyo na mikutano mingine yote Tume haikuweka na haitaweka ukomo wa idadi ya wananchi wanaopaswa kutoa maoni,” amefafanua Bw. Assaa na kuongeza kuwa Tume inatambua kuwa wananchi wana shauku kubwa ya kutoa maoni yao kuhusu Katiba Mpya.

Hata hivyo, Katibu huyo alisema kuwa ingawa Tume ingependa kumfikia kila mmoja mahali alipo, jiografia ya nchi na muda ambao Tume imepewa, jambo hilo halitawezekana na kuwasihi wananchi kujitokeza kwa wingi katika maeneo ambayo Tume itafanya mikutano kama ratiba iliyotolewa inavyoelekeza.

Akifafanua kuhusu malalamiko kuwa baadhi ya Kata hazitafikiwa na Tume, Bw. Assaa amesema Tume haikupanga ratiba ya mikutano ya kukusanya maoni haikupangwa kwa kuzingatia Kata, bali imepangwa kwa kuzingatia eneo ambalo linaweza kujumuisha wananchi kutoka zaidi ya Kata moja.

Pamoja na kutoa maoni yao kupitia mikutano, Tume pia imewaomba wananchi kuendelea kutumia fursa nyingine kuwasilisha maoniyao kama tovuti ya Tume (www.katiba.go.tz), barua pepe (maoni@katiba.go.tz) au kwa njia ya posta kupitia Tume ya Mabadiliko ya Katiba, S.L.P. 1681, Dar es Salaam na S.L.P. 2775, Zanzibar.     

Tume ya Mabadiliko ya Katiba ilianza kufanya awamu ya kwanza ya mikutano ya kukusanya maoni ya wananchi katika mikoa minane tarehe 2 Julai mwaka huu na inatarajiwa kumalizika tarehe 30 mwezi huu. Mikoa hiyo ni Dodoma, Kagera, Kusini Pemba, Kusini Unguja, Manyara, Pwani, Shinyanga na Tanga.
Reviewed by crispaseve on 03:22 Rating: 5

No comments

Post AD